Wakati
magari 150 ya msafara wa ziara ya Rais Barack Obama yamewasili nchini,
majina ya mawaziri wa Tanzania yatakayoruhusiwa kumpokea kiongozi huyo
kuchujwa na makachero wa FBI.Mkurugenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mwalimu
Julius Nyerere, Moses Malaki amesema kuwa matayarisho ya ujio wa Rais
huyo ni kabambe na hayajawahi kutokea katika historia ya Tanzania.Pia
alisema shughuli za kumpokea Rais Obama, anayetarajiwa kutua Jumatatu
saa 8:40 mchana, zitaanza asubuhi kwa maofisa wa Marekani kushika
majukumu yote katika uwanja huo, ikiwemo kuongoza ndege, ukaguzi wa
abiria na mizigo, kwa maana wafanyakazi wa uwanja huo kuwa likizo kwa
siku mbili.
Imebainika kuwa
hata idadi ya maofisa wa Tanzania wakiwemo viongozi watakaompokea pia
itapangwa na Wamarekani wenyewe.“Wenyewe wana orodha yao na wanajua nani
atakuwepo au hatakiwi kuwepo katika kundi la wageni watakaompokea Rais
Obama,” alisema na kuongeza:“Nilimuuliza Ofisa Usalama wa Marekani iwapo
nitaweza kumwona Rais Obama, akaniambia: Utamwona ukibahatika kuwepo
kwenye orodha.”Waziri wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe naye alikiri
kuwa mawaziri wanaotakiwa kuwepo katika msafara wa kumpokea Rais Obama
ni wachache watakaochaguliwa tu na Wamarekani, baada ya kuyapitia na
kuyachunguza majina hayo kwanza kabla ya kuyakubali.“Hii sijawahi
kuiona, hata sisi wenyewe tunateuliwa na wakishayapitia wataamua, nani
aende au asiende,” alisema Chikawe.Taarifa za uhakika zinaeleza kuwa
ndege hizo zilitua jana saa 5:00 usiku, zikiwa na uwezo wa kubeba magari
zaidi ya 50 kila moja. “Hii ni historia, wamekuja marais wengi hapa,
lakini ukaguzi, ulinzi na matayarisho mengine kama haya hayajawahi
kutokea,” alisema Malaki.Alisema hivi sasa mazoezi ya kumpokea Rais huyo
uwanjani hapo yanafanyika ambapo bendi rasmi ya askari wa Tanzania
itakayotumbuiza siku hiyo, maofisa wa Marekani na viongozi wa TAA,
wanafanya mazoezi na kuelekezana jinsi watakavyompokea Rais
Obama.“Mazoezi haya yatatoa picha rasmi ya jinsi Rais huyo atakavyotua,
wapi bendi ikae, wapi maofisa wasimame, wapokeaji na msafara wake mzima.